SERIKALI
 imesema eneo linalogombewa na Malawi katika Ziwa Nyasa ni mali ya 
Tanzania na sasa imeziamuru kampuni za nchi hiyo zinazofanya utafiti wa 
mafuta kuondoka eneo hilo kuanzia jana.
Onyo
 hilo dhidi ya Malawi lilitolewa jana na Waziri wa Mambo ya Nje na 
Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe ambaye pia amesisitiza kuwa 
Tanzania itakuwa tayari dhidi ya tishio lolote la dhahiri au la kificho 
la kiusalama.
Hii
 ni mara ya pili Serikali kuionya Malawi katika mgogoro huo. Wiki 
iliyopita aliyekuwa Kaimu Kiongozi wa Shughuli za Serikali Bungeni 
Samuel Sitta alisema: “Tuko tayari kwa lolote dhidi ya Malawi.”
Sitta
 alitoa kauli hiyo alipokuwa akijibu Swali la Mbunge wa Mbozi Mashariki,
 Godfrey Zambi aliyetaka kujua kauli ya Serikali kuhusu mgogoro huo.
Jana,
 akiwasilisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara yake kwa mwaka 
2012/13, bungeni mjini Dodoma, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa 
Kimataifa, Bernard Membe alisisitiza kwamba eneo linalobishaniwa katika 
ziwa hilo lipo Tanzania.
Alisema
 pamoja na Jeshi la Ulinzi la Wananchi Tanzania (JWTZ) kuzipiga marufuku
 ndege za utafiti za kampuni hizo, bado zilikaidi na ndege tano zilitua 
katika eneo la Ziwa Nyasa.
“Serikali
 ya Tanzania inapenda kuzionya na kuzitaka kampuni zote zinazoendelea na
 shughuli za utafiti katika eneo hilo zisitishe mara moja kuanzia leo 
(jana),” alisema Membe.Alisema Serikali ya Tanzania iko tayari kulinda 
mipaka yake kwa gharama yoyote na haitaruhusu utafiti huo wa uchimbaji 
wa gesi na mafuta uendelee.
Alisema
 chini ya Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), wananchi wa Tanzania 
watakuwa salama dhidi ya tishio lolote la dhahiri au la kificho la 
kiusalama.
Kiini cha Mgogoro
Kuhusu
 kiini cha mgogoro, Waziri Membe huku akirejea historia ya mipaka tangu 
ukoloni, alisema ni hatua ya Serikali ya Malawi kushikilia msimamo kuwa 
eneo lote la Ziwa Nyasa lipo Malawi wakati Tanzania inashikilia kuwa 
mpaka upo katikati ya Ziwa.
“Wenzetu
 wanadai ziwa lote lipo Malawi lakini, nyaraka zilizotengenezwa na 
wakoloni wa Kiingereza mwaka 1928 na 1938 zinaonyesha kuwa mpaka wa ziwa
 hilo upo katikati,” alisema. Alisema hoja ya Tanzania ina nguvu 
kulingana na sheria za kimataifa kwa vile tatizo kama hilo linafanana na
 mgogoro uliokuwepo baina ya Cameroon na Nigeria.

0 comments:
Post a Comment