Sunday, August 12, 2012

Kitengo cha dawa asilia Muhimbili chagundua tiba ya Kisukari

Kitengo cha Utafiti wa Dawa Asilia cha Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, kimegundua dawa za asilia za aina tatu za kutibu magonjwa ya kisukari na kibofu cha mkojo.

Kitengo hicho ambacho kazi yake ni utafiti wa dawa asilia, kimefanikiwa kugundua dawa hizo katika kipindi cha miaka 38 tangu kuanzishwa kwake mwaka 1974.
Dawa zilizogundulika na kuonyesha mafanikio makubwa ni aina ya Morizela zilizopo kwenye mfumo wa juisi ambazo moja ina sukari na nyingine haina ambazo zimeonyesha mafanikio makubwa katika tiba ya kisukari.
Dawa nyingine ni aina ya Prucan ambayo hutibu wagonjwa wenye matatizo ya kutopata haja ndogo, magonjwa ambayo huwapata zaidi wanaume wazee.
Akizungumza na gazeti hili, Kaimu Mkurugenzi wa kitengo hicho, Dk. Ester Innocent, alisema pamoja na kwamba dawa hizo zimeshaanza kutumika, lakini bado hazijaingia sokoni kwa vile bado ziko kwenye Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA).
Alisema TFDA ikishatoa usajili wake, kitengo hicho kinaweza kuingia mikataba na wenye kampuni za kutengeneza dawa ili zizalishwe kwa wingi na kuwafikia wagonjwa wengi popote walipo.
Alisema kwa sasa dawa hizo zinapatikana kwa uchache sana kutokana na kuzalishwa hospitalini hapo na ikishapata usajili, itapatikana kwa wingi.
Kwa mujibu wa Kaimu Mkurugenzi huyo, pamoja na kitengo hicho kuanza muda mrefu na hatimaye mwaka huu kutoa rasmi dawa hizo, wengi wataona imechukuwa muda mrefu lakini akasisitiza kuwa utafiti kwa kawaida huchukuwa muda mrefu.
Dk. Innocent alisema watafiti mara nyingi ni wepesi kugundua tiba ya dawa, lakini dawa hiyo haiwezekani kutumika bila kujua madhara yake, hivyo wanalazimika kuanza tena utafiti wa kuyajua madhara hayo na kuyadhibiti.
Hata hivyo alisema zipo dawa nyingi za asili zinazofanyiwa utafiti lakini ambazo utafiti wake uko karibuni kukamilika ni za aina 11 zinazotibu magonjwa mbalimbali kama malaria, pumu, tumbo, ngozi na magonjwa nyemelezi ya ukimwi.
Alisema kitengo hicho kinakabiliwa na changamoto nyingi hasa za uhaba wa fedha na hivyo kujikuta kuchelewa kutoa matokeo ya tafiti zao kwa wakati.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

0 comments:

Post a Comment