Friday, August 17, 2012

Wabunge CCM Wahaha Kujikosha Na Ufisadi


TUHUMA za rushwa dhidi ya wabunge juzi zilitawala kikao cha Kamati ya Wabunge wa CCM, ambapo Waziri Mkuu Mizengo Pinda aliombwa kuingilia kati ili ‘kuwasafisha’ wenye tuhuma hizo mbele ya jamii. Kikao hicho kiliitishwa pamoja na mambo mengine, kuzungumzia nafasi ya wabunge wa CCM katika kuhamasisha umma kushiriki katika Sensa ya Watu na Makazi itakayofanyika Agosti 26, mwaka huu na utoaji wa maoni kwa Tume ya Katiba Mpya.

Habari kutoka ndani ya kikao hicho, zimesema pamoja na kwamba haikuwa moja ya agenda za mkutano huo, Mbunge wa Bukene, Seleman Zedi alisimama na kuibua kilio cha wabunge wanaotuhumiwa kwa rushwa. Mbunge huyo ambaye pia alikuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini iliyovunjwa na Spika wa Bunge, Anne Makinda alimweleza Waziri Mkuu kwamba baadhi ya wabunge, hasa wa iliyokuwa kamati yake, wangekwendaje kuhamasisha Sensa majimboni wakati wamechafuka kwa tuhuma za rushwa?

Mtoa taarifa wetu anasema, mbunge huyo akiungwa mkono na Mbunge wa Viti Maalumu, Munde Tambwe, walimwomba Waziri Mkuu ambaye ni mwenyekiti
wa kikao hicho, amweleze Spika awasafishe kwa kutangaza bungeni kwa madai kuwa tuhuma dhidi yao hazikuthibitika.

Alisema kauli hiyo ya Spika ingewasaidia kurudi majimboni wakiwa wasafi na wenye mamlaka ya kimaadili kuungana na wenzao kuhamasisha Sensa na utoaji wa maoni ya Katiba Mpya. Hata hivyo, vyanzo vyetu vya habari vimetofautiana kuhusu kauli ya Pinda baada ya kupokea malalamiko hayo, kimoja kikisema alikaa kimya na kingine kikisema alijibu kuwa asingeweza kuingilia kati suala hilo kwa kuwa bado linachunguzwa na Kamati ndogo ya Bunge. Mambo mengine yaliyoibuka kwenye kikao hicho ni mjadala wa Muswada wa Fedha.

Wabunge wa CCM walipinga ongezeko la kodi kwenye maji ya kunywa na msamaha wa Kodi ya Ongezeko la Thamani (Vat) kwa kampuni za kuchimba madini. Kwa zaidi ya wiki sasa, Kamati ndogo ya Bunge iliyoundwa na Spika Makinda imekuwa inaendelea kuwahoji baadhi ya wabunge ama wanaotuhumiwa au wenye ushahidi wa tuhuma hizo. Baadhi ya wabunge wamekuwa wakiitwa mmoja baada ya mwingine na kuhojiwa na wajumbe hao faragha kuhusu ama madai ya rushwa dhidi yao au mambo waliyoeleza kuhusu tuhuma hizo. Tuhuma hizo zilisababisha Spika Makinda kuvunja Kamati ya Nishati na Madini iliyodaiwa kukithiri kwa rushwa.

0 comments:

Post a Comment